Friday, June 15, 2012

Hatujadhamiria kupambana na umasikini nchini.


 Na: John Alex.

“Kama kila mmoja wetu angefagia nje kwake basi bila shaka dunia nzima ingekuwa safi”Haya ni maneno ya mtawa mmoja wa dini ya kikristo kutoka dhehebu la katoliki ajulikanae kwa jina la mama Theresa aliyewahi kuishi huko barani Asia nchini India,maneno ambayo leo nimeona nianze nayo.

Napenda sana kutumia mifano nikirejea maisha ya watu wa kipato cha chini ambao ndio walio wengi hapa nchini Tanzania hususan wakulima waishio maeneo ya vijijini na kama nikiwagusa   mijini basi napendelea wale waishio uswahilini maeneo ambayo ndio yanatoa taswira ya maisha halisi ya mtanzania.Achana na wale waishio mitaa ya  Masaki,Ostabei huko Dar es salaam,na kama ni mkoani Iringa basi waishio Wilolesi,na Igangilonga hawanihusu leo hii.

Bahatika siku moja kutembelea maeneo ya uswahilini,halafu kule chunguza kwa makini sana maeneo ambayo watu wanapenda kukusanyika wakiongea mambo mbali mbali,utapata majibu ambayo kwa sehemu fulani  yataendana na haya ya kwangu.

Uswahilini bwana,saluni za kiume  hufurika vijana ambao asilimia kubwa unawakuta wakisikiliza muziki wa kizazi kipya wala hawaendi kunyoa kwa sababu wengi wao utawaona na rasta kichwani.Hii iko sana  mijini tena utawakuta wengine maeneo ambayo wameyapa majina kama vile  kijiweni,kempu saiti na kadhalika na huko unawakuta wakiburudika na bangi ambayo imepewa majina  kama  vile Kaya,Widi,Mjani. na Ganja.

Kijjini  nako kuna wanaume wenye nguvu zao wasio na aibu ambao hawafanyi chochote na badala yake kuanzia asubuhi mwanzo mwisho utawakuta wakipiga mambo yetu yale,sasa kama ni hapa Iringa  au Mbeya ni Ulanzi ndio namaanisha.Kama  wangekuwa Ujerumani kipindi cha Adolf Hitler  wasomaji mashahidi watu kama  hawa ambao waliitwa kwa lugha ya kiingereza(unproductive) walikuswanywa vizuri tu na kutupwa baharini ama  walichomwa moto kwenye cchumba cha gesi.Na hii iliwatia adabu wajerumani wakati huo na matokeo yake nchi iliendelea na matokeo yake ikapata kiburi cha kuitawala dunia fuatilia historia  ya ujerumani.

Sasa huyu mwanamke  naye kaolewa na ni mama wa nyumbani,hana shughuli yeyote  ya kumuingizia kipato kamuandaa mumewe  kwenda kazini asubuhi ,kamvalisha mtoto tayari kumpeleka  kwenye kajinasari  jirani tu na nyumbani akisharudi mwanamke hatulizi miguu nyumbani asubuhi hiyo hiyo anasugua kisigino huyo! mpaka nyumba ya jirani,akifika kwa shoga yake wanatoa jamvi nje wanaanza kupeana michapo na mbaya zaidi  wengine wanavuka   mpaka mambo ya ndani  wanashea pamoja.Aaah! ndio mambo ya wanawake hayo. “Tutafanyaje na wakati huku mjini uswahilini nyumba zimebanana hata kufuga kuku tu ni inshu chumba chenyewe ni kimoja”Jamani hata  kuuza maandazi pia au kufuma vitambaa! kwani kuuza genge vipi?

Kwa mtazamo wangu nafikiri elimu ya uzazi wa mpango hususan baadhi ya maeneo  huko vijijini bado kabisa haijawafikia  na kama imewafikia basi hawajaielewa sawa sawa kwa sababu inakuaje  wanandoa wanazaa kila mwaka mtoto jamani? Inafikia kipindi familia unakuta ina watoto nane na kuendelea.Kibaya zaidi hembu kwa nje tu angalia afya ya mama na mtoto ilivyo ya kusikitisha! Mzee naye kachoka kweli kweli anategemea biashara ya mkaa na kuwalisha watoto na mama yao tu ni inshu siku nyingine wanashindia uji,nyumba ni ya nyasi tena wala dirisha haina na inakaribia kuanguka mchwa washafanya kazi yao.Kali zaidi watoto watatu wa mwisho  wana shinda  na chupi tu wengine ndio kidogo wana kaptura na wa kiume wakubwa  kidogo mashati ya baba yao ya zamani ndio wanajisitiri. Choo nacho kilishajaa siku nyingi na ukienda kusabahi hapo muda wowote angalia sana usije ukakanyaga kinyesi cha watoto.Kwa hili nasema watanzania  wote na serikali yetu  hatupo siriasi na hili swala

Huyu naye  anajiita sharobaro.Ni kijana, yuko stendi ya daladala na wala sio kuwa anasubiria Gari kaja kung’aa macho tu na kushangaa shangaa hana lolote.Anasogea kando ya barabara pembeni kidogo  kuna fundi viatu.Anaanza kucheka haalafu anasema; “Mimi bwana hata kama nimefika  darasa  la saba  kuna kazi nyingine  kufanya ni kama kujichoresha tu mchizi anashona viatu dah!kweli jamaa kauzu”

Hembu ona sasa hata darasa la saba naye katika ulimwengu huu wa leo anachagua kazi eti! Kama sio kunyonyana katika jamii ni nini huku.Kuna kauli ya wahenga inasema  mtembea bure si sawa na  mkaa bure. Sasa watu kama hawa  ambao wanaendekeza uvivu ikiwa hawana ujuzi wowote  na wala hawataki kuwa wabunifu,wala hawako tayari kujituma kufanya kazi kwa lengo la kuepuka kuwa  tegemezi  sikosei kuuita mzigo katika jamii  na serikali kwa ujumla.

Siku zote  ukitaka kutoa kibanzi  kilichoko ndani ya jicho la mwenzako basi ni vema na ni jambo la busara kama  ukianza kutoa boriti jichoni mwako kwanza na  kisha uanze sasa kukitoa cha huyo mwenzio.Namaanisha nini ?Ni kwamba wananchi wa Tanzania walio wengi tumekuwa tukiitupia lawama serikali pasipo kukumbuka  kuwa maendeleo katika taifa hili huletwa na wananchi wenyewe na serikali ni kama msimamizi tu.

Hapa msomaji naomba unielewe simaanishi kuwa serikali hawana mapungufu. Wanayo. tena makubwa tu.Usimamizi mbovu wa rasili mali nchini,ufisadi unaofanywa na baadhi ya viongozi waliokosa uzalendo kwa taifa lao ambao wapo katika kutetea maslahi yao binafsi pasipo kujali  dhamana waliyopewa kuwatumikia watu  kwa kuzingatia  haki na usawa,pamoja na rushwa kubwa  iliyokithiri haya yote ni mzigo wa serikali.Sasa mimi leo nataka kila mmoja abebe mzigo wake hapa.

Vitabu vya dini karibia zote ulimwenguni  vimekuwa vikihimiza watu kufanya kazi kwa bidii na vingine vikiandika siri ya mafanikio ni   kujituma na kinyume na hapo huwezi kufanikiwa.Sasa kauli hii nayo inatoka katika Biblia,moja ya vitabu vya dini na inasema “Asiyefanya kazi na asile”

Leo nataka tuangalie umasikini kama tatizo la kijamii  na nafasi ya  jamii katika kupiga vita umasikini ambao madhara yake yamekuwa yakishambulia sana  jamii za  kitanzania  ambazo kwa nafasi yake pia jamii hizi zimekuwa zikijisahau kwa sehemu katika kulikabili tatizo aidha kutokana na kutojali ama kwa kukosa tu maarifa.Aidha mchango  anaoutoa mtu moja moja katika shughuli za kujiletea maendeleo unatolewa kikamilifu?
Umasikini kama tatizo la kijamii hugusa kila nyanja  katika maisha  ya binadamu ya kila siku.Hujumuisha  kipato kidogo kwa wanajamii,ukosefu wa huduma stahiki za kijamii kama vile maji umeme,hospitali,ukosefu wa mahitaji muhimu ya binadamu kama vile chakula mavazi na  malazi lakini pia  uwezo mdogo wa kufanya maamuzi  utokanao na  ujinga uliokithiri miongoni mwa jamii zetu za kitanzania,pia umasikini wa kiroho ambao humfanya mtanzania afikiri mawazo duni,awe ni mtu wa kukata tama,,na mwenye kujiona hawezi kufanya kitu chochote.

Asilimia kubwa mtakubaliana na mimi kuwa watanzania walio wengi katika jamii zetu tunamoishi  tumeshakata tamaa na tumeridhika kabisa na tulichonacho hata kama ni duni.Mbaya zaidi mwingine karidhika kabisa na  kukosa na hatimae kujikuta tukiishi maisha yasiyokuwa na muelekeo wowote kwani ni mara ngapi unakutana na watu waliokata tamaa na maisha  na wengi wetu tunafikiri hawa labda wamechanganyikiwa  kutokana na muonekano wao wa nje.Hii inatokana na uwezo duni wa kufanya maamuzi.

Kwa upande wavijana katika jamiii tunashindwa kuthubutu kufanya mambo ambayo kwa namna moja ama nyingine tunaamini kabisa kuwa  hatuwezi kutokana na mitazamo hasi ambayo imepandikizwa na waliotutangulia kwa maslahi yao.

Uvivu ni jambo ambalo linatawala vjana wengi wa kitanzania katika dunia hii ya leo na kushindwa kufanya  chochote  na ndio maana  matokeo yake tunashindwa kutumia fursa zinazojitokeza kwa manuufaa yetu wenyewe.

Zipo fursa nyingi mitaani ambazo kwa  vijana ambao kutokana na sababu mbalimbali za msingi na zisizo za msingi wamekosa fursa ya kuendelea na masomo yaani wameishia  darasa la saba,ama  kidato cha nne wanaweza kuzitumia ipasavyo badala ya kuzidharau kujletea maendeleo ili kuepukana na tatizo kubwa la kuwa tegemezi.

Kwa akina mama ni muda muafaka sasa kuachana na mawazo na fikra mgando ambazo kwa maoni yangu zimepitwa na wakati.Fikra kama vile mwanaume peke yake ndiye mtafutaji mwanamke anabaki nyumbani.Na kwa wale dada zangu huu sio wakati wa kusubiria kuolewa kwani saasa hivi wanaooa wanatafuta mtu anayejituma na mchapa kazi,kinyume na hapo hutoolewa labdaumpate mvivumwenzio.Wakina dada tuepukane na hili tusije  tukaishia kufanya biashara za ajabu mtaani .Baadhi ya akina dada hawakawii.

Ni vema watanzania wakaeleweshwa kwa mapana juu ya hali halsi ya kiuchumi namabadilikoyanayotokea ulimwenguni kote.Katika kipindi hiki cha mabadiliko watanzania kila mmoja kwa nafasi yake atambue nafasiyake katika kuleta maendeleo,badala ya kutegemea serikali ambaayo na yenyewe  kwa kweli inakosa muelekeo kila kukicha

Tukumbuke kuwa sisi ni matunda ya kizazi kilichopita na sio wafungwa  wa kizazi kilichopita.Hivyo uwezo wa kuleta mabadiliko kuanzia ngazi ya familia kijiji  mkoa na taifa  upo mikononimwetu iwapo tu kila mmoja wetu kwa nafasi yake atashiriki kikamilifu katika kuleta mabadiliko.
Watanzania tukumbuke kuwa nchi nyingi ambazo leo hii ndio nchi wahisani,nchi zinazoitwa nchi zilizoendelea zilipita katika kipindi kigumu  kama hiki lakini baada ya kukubali matokeo na hatimae leo hii wanafaidi  matunda ya  juhudi zao.

Nijukumu letu sasa kuhakikisha kuwa tunaondokana na fikra za woga wa kuleta mabadiliko katika jamii,na badala yake tuvae ujasiri tukidhamiria kuleta  maendeleo katika nyanja zote katika taifa hili.

Yote haya yatafanikiwa endapo tutarejea na kuifanyia kazi kauli hii ya kila moja kufagia nje kwake na hatimae baadae tutajikuta tukiishi katika Tanzania yenye siasa safi,uongozi bora  na watu wote kunufaika na rasilimali za nchi na hivyo kupata fursa sawa kwa wote kattika kushiriki ujenzi wa taifa letu Tanzania





















             








No comments:

Post a Comment