Saturday, December 17, 2011

Mkuu wa wilaya Iringa ashauri ufugaji wa nyuki kisasa

Na John Alex.
           
Wananchi wa mkoa wa Iringa wameshauriwa kufuga nyuki kwa njia za kisasa na za kitaalamu zaidi ili kuweza kujikwamua kutokana na hali ngumu  ya kimaisha na hivyo  kupiga hatua katika  vita dhidi ya umasikini na kujiletea maendeleo.

Hayo yamebainishwa  na mkuu wa wilaya ya Iringa mjini Asley Msangi katika kikao cha kamati ya ushauri (DCC)cha manispaa ya Iringa  kilichofanyika mwishoni mwa wiki ilyopita katika ukumbi wa manispaa ya Iringa.

Mkuu wa wilaya amesema kuwa wapo wananchi wanaoishi kwa kutegemea    ufugaji wa nyuki na hivyo ni vema wananchi wakaanzisha miradi ya  ufugaji nyuki kwa  njia za kisasa na za kitaalamu zaidi na hivyo kujipatia faida kupitia miradi hiyo.

Aidha mkuu wa wilaya ameishauri idara husika ya manispaa ya Iringa kuandaa mikakati madhubuti ya kuwezesha wananchi kujifunza namna ya kufuga nyuki  kwa njia za kisasa na za kitaalam zaidi na   hivyo kuweza kujipatia faida kubwa kutokana na  mazao ya nyuki.

“Wananchi endapo wataamua kufuga nyuki kwa njia za kisasa na za kitaalamu wataweza kuinua zaidi kipato chao kwani mazao ya nyuki kama vile asali n anta yana soko sana na bei yake imekuwa ikipanda kila kukicha”alisema mkuu wa wilaya.

Amesema kuwa  ni wakati  muafaka kwa wananchi kuhamasika kufuga nyuki kwa njia za kisasa na za kitaalamu zaidi na  kwa kushirikiana na idara husika  ya nyuki ya manispaa, kuhakikisha  kuwa miradi ya nyuki inatekelezwa kwa kiwango kinachotakiwa  kwani ni njia mojawapo ya kuondokana na umasikini katika taifa letu.

Mkuu wa wilaya amesema kuwa  kwa muda mrefu idara husika ya nyuki ya manispaa ya Iringa  imekuwa  ikisuasua  sana katika  uhamasishaji wa miradi ya  ufugaji nyuki kwani kuna muitikio mdogo sana wa wananchi katika swala zima la ufugaji wa nyuki kwa wakazi wa manispaa ya Iringa

Ameishauri  idara hiyo ijifunze namna ya ufugaji nyuki kwa njia za kitaalamu na za kisasa na hivyo kuwaelimisha na kuwahamasisha wanachi ufugaji wa nyuki kwa njia za kisasa zaidi ili kuwezesha wananchi wa manispaa ya Iringa wanaojihusisha na ufugaji wa nyuki kupata kwa wingi mazao ya nyuki na hivyo kujikwamua na umasikini.


No comments:

Post a Comment